Nyusi zangu zinakutana katikati

Lakini sijali

Nimekuwa na nyusi nyingi na hazikunisumbua nilipokuwa mdogo, lakini hivi majuzi sikuweza kujitazama kwenye kioo bila kuzichukia!

Jambo ni hili, nina umri wa miaka 14 na tangu nianze hedhi zangu na kubalehe, mwili wangu ulipitia mabadiliko makubwa – baadhi sikuyafurahia. Ninafurahia kwamba kwa sasa matiti na mavuzi yangu ni madogo, lakini sikufurahia kwamba nilikuwa nimemea nywele kwenye uso na nyusi zangu zilishikana katikati mwa uso kama kiwavi mkubwa usoni (hivi ndivyo baadhi ya watoto shuleni walivyosema!).

Nilitamani sana kuondoa nywele zilizomea usoni na kugawanyisha nyusi zangu, kwa hiyo nikamuomba mama yangu ushauri. Alinielewa vyema na akanielezea kwamba ubalehe ni wakati ambapo mwili hupitia mabadiliko mengi ya kimwili na hisia na wakati mwingine huwa pandashuka, lakini unapaswa tu kujikaza na kuupitia. Alinielezea homoni ni nini na jinsi zinavyofanya kazi – ni kemikali maalum mwilini mwako ambayo hutuma taarifa za kudhibiti matendo ya mwili wako, kama vile njaa na hisia. Wasichana wanapobalehe miili yao hutoa homoni zinazoitwa estrojeni na ya wavulana huitwa testosterone.

Pia alinielezea kwamba sisi wote ni tofauti na tunaathiriwa tofauti na homoni zilizo ndani yetu – wengine watapata chunusi, nywele za mafuta mengi, mihemko ya hisia kama vile kuwa na furaha au huzuni au kumea nywele kwenye uso (kama mimi!). Alisema kwamba kufanya jambo la ghafla wakati mwili wetu unakua linaweza kuwa jambo utakalojutia baadaye.

Tulizungumza jinsi nilivyohisi wasiwasi kwa sababu ya watoto walionichokoza shuleni. Mama yangu alinifanya niangalie kwenye kioo na niseme kwa nguvu, “Mimi ni mrembo jinsi nilivyo, ndani na nje.” Ilinifanya nihisi vizuri kuhusu mimi mwenyewe. Sasa mimi huimba maneno haya kila asubuhi ninapojitayarisha kwenda shule na yamenisaidia sana kuelewa kwamba mimi ni mrembo jinsi nilivyo – nyusi zangu nyingi zinapendeza. Kwa sababu ni sehemu ya yanayonifanya niwe wa kipekee!

Sasa ninajihisi vyema zaidi na ikiwa kuna atakayenichokoza tena, mimi hutabasamu na kusema, “Ahsante kwa kugundua jinsi nilivyo mrembo na wa kipekee!”

Share your feedback