Nilikuwa na ndoto kubwa lakini sikujua jinsi ya kuitimiza...

Hadi nilipofuata vidokezo hivi 4

Wengi wetu tuna ndoto za kufanikisha kitu fulani kipya kama vile kuwa wa kwanza katika somo la Hisabati darasani mwetu au kugeuza uraibu wetu wa kuandika kuwa taaluma siku moja. Lakini ni vigumu kujua jinsi ya kutimiza ndoto hiyo. Tina alikuwa katika hali kama hiyo lakini alifanikiwa kukabiliana nayo. Ifuatayo ni hadithi yake.

“Mimi ni Tina na nimekuwa mwenye haya kila wakati. Mimi hujihisi huru ninapokuwa miongoni mwa wanafamilia wangu, lakini katika makundi makubwa mimi huwa mwenye uoga na kukosa maneno ya kutamka. Ukweli ni kuwa, kila mara nimetaka kuwa mwalimu. Ninapenda kutumia muda wangu kukaa na ndugu na dada zangu wadogo na kuwasaidia kufanya kazi zao za nyumbani na kuwafunza mambo mapya. Ninapenda kuwaona wakiongeza kiwango chao cha ujuzi na kujiamini. Hata hivyo, sikuhisi kama nina ujasiri ndani yangu wa kufunza na kisha kusimama mbele ya darasa zima!

“Mchana mmoja, nilichelewa kutoka shuleni kwa sababu nilitaka kupata muda wa kuwa pekee yangu na mwalimu wangu ninayempenda. Nilimwelezea kuhusu hali yangu na kuwa nilihisi kuwa zile ndoto zangu za kuwa mwalimu kama yeye hazikuwa na matumaini. Mwalimu wangu alinieleza kuwa sipaswi kusikiliza hizo sauti hasi zinazoniambia kuwa siwezi kufanikiwa, lakini ninapaswa kusimama na kufanya kazi ili kutimiza ndoto zangu. Alinisaidia kujihisi mwenye ujasiri na kujivunia ujuzi nilionao na mtu ninayetaka kuwa.

“Wiki lililofuata niliketi chini ili kutengeneza mpango. Kwanza, mwalimu wangu aliniomba kuchanganua ndoto yangu kuwa katika malengo madogo mdogo ya kuweza kutimiza hatua kwa hatua. Pili,alinisaidia kutambua ujuzi ambao ningehitaji kuboresha ili kuwa mwalimu, kama vile kiwango changu cha kujiamini. Niliamua kutumia muda wangu kumsaidia kufanya kazi za madarasa ya chini ili kukuza kiwango changu cha kujiamini mbele ya makundi. Tatu, alinishauri kutafuta kozi za ualimu katika eneo langu. Kwa mafano huenda kukawa na kozi za ualimu ambazo zinaweza kulingana vizuri na gredi zangu za shuleni kuliko zingine. Mwisho, alikubali kuwa mshauri wangu ili kunisaidia kufuata malengo yangu.

Vidokezo vya mwalimu wa Tina vilisababisha mabadiliko yote. Je, unahitaji ushauri ambao unaweza kuuamini? Jaribu vidokezo hivi…

1. Tafuta mtu anayefaa wa kuzungumza naye:

Mtu unayemjua na unayejihisi huru kuwa naye, kwa sababu kuna uwezekano mkubwa kuwa wanaweza kuona matatizo yako kutoka kwa mtazamo wako.

2. Andika kila kitu unachostahili kupata ushauri kukihusu:

Hatua hii itakusaidia kuelezea hisia zako kwa njia bora na kupata ushauri sahihi kwa mtu utakayemwendea ili kupata ushauri.

3. Chagua muda bora wa kuanzisha mazungumzo:

Ni wewe unayedhibiti wakati, mahali na jinsi. Mwulize pia mtu unayetaka kuzungumza naye muda bora unaomfaa.

4. Sisi sote tuna maoni yetu:

Huenda ukapenda baadhi ya ushauri, ushauri mwingine huenda usikufae. Licha ya hivyo, mshukuru mtu kwa kukupa muda wake na kuwa unashukuru kwa usaidizi wake. Unaweza kutathmini ushauri wao na hisia zako mwenyewe kwa muda.

Share your feedback